WAUZIWA NYAMA YA FISI BILA KUJUA




WAKAZI wa eneo la Madogo, kaunti ya Tana River wameonywa wawe macho dhiidi ya watu wanaodaiwa kuuza nyama ya fisi kwa bei rahisi wakiwahadaa raia kwamba ni nyama ya ng’ombe.
Kulingana na chifu wa eneo hilo, Bw Aaron Kunyo nyama hiyo inaaminika ni ya fisi ambao idadi yao ni kubwa katika eneo hilo. Alisema wakaguzi wa nyama wamekuwa wakikosa kugundua nyama hiyo ambayo sasa inauzwa kwa bei nafuu ya Sh40 kwa kilo moja ikilinganishwa na nyama halisi ya ng’ombe ambayo bei yake ni Sh120 kwa kilo.

“Imekuwa ikiuzwa vichochoroni hasa kuanzia saa kumi na moja asubuhi hadi saa saba mchana. Wauzaji wamekuwa wakiificha katika mabandali ya unga,” alisema Bw Kunyo.

Chifu huyo ilisema msako wa dharura uliofanywa na afisi yake na wakazi ulipelekea kukamatwa kwa mtu mmoja ambaye alikuwa akiuza nyama inayoaminika kuwa ya fisi.

Mtu huyo ambaye alikamatwa akiwa na kilo 90 za nyama alipatikana na ngozi ya mnyama huyo wa mwitu.

“Tumepeleka sampuli za nyama hiyo kwa maabara ya serikali na punde tu baada ya matokeo kutolewa, mwanamume huyo atafunguliwa mashtaka,” alisema Bw Kunyo.

Ripoti hizo zimezusha hofu miongoni mwa wakazi wa eneo hilo ambao wengi wao ni waislamu. Kulingana na tamaduni za wakazi wa eneo hilo, mtu akila nyama za mnyama yeyote wa mwituni hupata laana na mifugo wake wanaweza kufa wote.

Mzee Juma Bagana, mkazi wa eneo hilo, alisema shida hiyo imesababishwa na ukosefu wa kichinjio katika eneo hilo. Alisema wauzaji nyama na wenye hoteli hutengemea kichinjio cha mjini Garissa.

Matapeli
“Serikali ya kaunti ya Tana River inapaswa kuharakisha mipango ya kujenga kichinjio hapa Madogo ili kuwakinga wakazi dhidi ya matapeli wanaowahadaa. Hilo likifanywa, tutaweza kuwachinja wanyama wetu hapa, nyama ikaguliwe na tununue nyama iliyothibitishwa kuwa salama,” alisema Mzee Bagana.

Tukio hili limeibua kumbukumbu katika nchi jirani ya Somalia ambako wanamgambo wa Al Shabaab walianza kuwauzia nyama ya fisi watu wa maeneo waliyoyadhibiti ili kuchangisha pesa za kufadhili shughuli zao.

Kulingana na kundi hilo, nyama ya fisi hutumiwa kwa kuvunja laana na pia kuwaepusha watu dhidi ya magonjwa.

Hata hivyo, viongozi wa dini ya kiislamu kwa muda mrefu wamesisitiza msimamo wa kuwakataza waumini wao dhidi ya kula nyama ya fisi hsa ikizingatiwa kwamba mnyama huyo hula mizoga ya wanyama wengine na pia binadamu.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo