
Akitoa
taarifa hiyo mjini Abuja, balozi huyo, Bw Tagelsir Mahgoob Ali,
aliwaambia wanahabari kuwa rais huyo alikuwa amepanga kukutana na marais
wengine watatu wakiwemo, rais Goodluck Jonathan wa Nigeria, waziri mkuu
wa Ethiopia Hailemariam Desalegm na rais wa Kenya Bw Uhuru Kenyatta.
Hili alisema ndicho kilikuwa kiini cha kutokuwepo kwake. Bw Al-Bashir
alikuwa nchini Nigeria kwa mwaliko wa Umoja wa Afrika(AU) katika
kongamano maalum kuhusu Ukimwi na Malaria.
Muungano huo
umepitisha azimio linaloyakataza mataifa wanachama kumkamata rais yeyote
aliye afisini na anayekabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kivita katika
mahakama ya ICC.
Balozi huyo
alisema kuwa ni baada ya kuandaa mkutano katika ubalozi huo ambapo
alionelea kurudi nchini Sudan, kwani hakukuwa na jambo lingine muhimu
lilikuwepo ambalo lingemfanya kubaki nchini Nigeria kwa siku ya pili.
Aidha, balozi
huyo alisema kuwa rais Bashir alimtuma waziri wake wa afya kusoma
hotuba kwa niaba yake, huku akifanya mashauriano na marais hao watatu
katika vikao tofauti.
Balozi huyo
alisema kuwa Bw Bashir hajawahi kuwa na wazo lolote la kuogopa kukamatwa
akiwa nchini Nigeria, huku akiongeza kuwa Nigeria ilikuwa mojawapo ya
mataifa yaliyopinga ubaguzi wa ICC barani Afrika.” Ikiwa Nigeria
ingeusikiza wito wa ICC, ingejitokeza vipi kama mojawapo wa nchi
zinazopinga mwingilio wake barani Afrika,” akasema Bw Ali.
Kando na
hayo, alionya kuwa ikiwa Al- Bashir 'angeanguka’, ni kama bara la Afrika
limeanguka. Balozi huyo alisema kuwa Afrika sharti ikatae juhudi za
nchi za Kimagharibi kuleta ukoloni mamboleo. Alisema kuwa mahakama ya
ICC imekuwa fimbo ya kisiasa, na kwa hivyo mataifa ya Afrika sharti
yaikatae. Alitia shaka 'kujitolea’ kwa nchi za Magharibi katika
kukabiliana na Ukimwi na Malaria.
NA AFP