susan-rice.si
Rais Barack Obama wa Marekani amemteua mshirika wake wa muda mrefu Susan Rice kuwa mshauri wake mkuu wa masuala ya usalama, nafasi ambayo haihitaji kuthibitishwa na baraza la Seneti. 

Wakati akiwa katika nafasi yake ya zamani kama Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Rice aliingia matatani kuhusiana na maelezo yaliyotolewa na utawala juu ya shambulizi dhidi ya ubalozi mdogo wa Marekani mjini Benghazi Libya, mwaka uliyopita.

Wapinzani wa chama cha Republican walimtuhumu Rice kwa kutoa taarifa za upotoshaji zenye lengo la kuficha ukweli. 

Rais Obama amemsifu Rice kama mtumishi wa umma aliekamilika, mzalendo ambae hutanguliza nchi yake, jasiri na anaye elewa kuwa hakuna mbadala kwa uongozi wa Marekani. 

Obama pia amemteua Samantha Power, mtaalamu wa haki za binaadamu, kuwa balozi mpya katika Umoja wa Mataifa. 

Uteuzi wa Samantha Power lazima uthibitishwe na baraza la Seneti.