Katibu
Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bw. Ban Ki-Moon ameikosoa sheria mpya
iliyopitishwa na serikali ya Burundi, ambayo amesema itaathiri uhuru wa
vyombo vya habari.
Mapema
wiki hii Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi aliiridhia sheria hiyo,
ambayo imekosolewa na mashirika ya habari na yale ya haki za binaadamu.
Msemaji
wa Umoja wa Mataifa Martin Nesirky, amesema Katibu Mkuu Bw. Ban Ki-Moon
amesikitishwa na sheria hiyo, yenye vifungu vinavyoweza kukandamiza
uhuru wa habari, huku akisisitiza kuwa haki ya uhuru ya kujieleza na
sekta huru ya habari ni mambo muhimu kwa ustawi wa demokrasia.
Sheria
hiyo iliyopitishwa na bunge la Burundi mwezi April, inadhoofisha ulinzi
wa vyanzo vya habari, inadhibiti kuripoti habari za uchunguzi na
inawataka waandishi wote kuwa na shahada ya Chuo Kikuu bila kujali
uzoefu.
Pia
inapiga marufuku kusambaza taarifa au nyaraka kuhusu mada za ulinzi au
taarifa zinazochukuliwa kuwa propaganda za adui, au zinazoweza kuathiri
uchumi wa Burundi.