![]() |
| Mwalimu mkuu Godigodi Malangalila |
Shule ya msingi Ndulamo iliyopo kijiji cha Ndulamo wilayani
Makete ipo hatarini kukumbwa na magonjwa ya milipuko kama kipindupindu na
kuhara kutokana na ukosefu wa maji, hali inayowalazimu wanafunzi kujisaidia
kwenye vyoo vya shule hiyo bila maji
Akizungumza na mtandao huu ofisini kwake mwalimu mkuu wa
shule hiyo Bw. Godogodi Bosco Malangalila amesema tatizo hilo limekuwa sugu
shuleni hapo hivyo linahatarisha usalama wa wanafunzi na wakati mwingine hadi
waalimu
Amesema tatizo hilo linahatarisha afya za wanafunzi wake kwani
pamoja na ukosefu huo wa maji wakati mwingine shule hulazimika kuvunja vipindi
na kuwaagiza wanafunzi kwenda kuchota maji kwenye mito ama visima ambayo si
safi na salama kwa matumizi ya binadamu lakini wao hulazimika kuyatumia hivyo
hivyo
“Ndugu mwandishi inasikitisha kwa kweli, hapa shuleni huwa
tunatoa uji kwa wanafunzi lakini maji hata ya kuosha vyombo hakuna, ya kutumia
vyooni nayo hakuna na vyoo vya shule ni vile vya kutumia maji, lakini wanafunzi
huenda kujisaidia hivyo hivyo bila maji” alisema Mwalimu Malangalila
Ameongeza kuwa mara nyingi vyoo hivyo huziba na kulazimika
waalimu wenyewe kuvizibua vyoo hivyo na wakati wengine kuwaita wazazi kuja
kuzibua vyoo hivyo lakini hivi sasa wazazi wengi hugoma kuja kufanya shughuli
hiyo kwa madai kuwa wao wanachanga fedha za maji kijijini hivyo ni jukumu la
vyombo husika kufikisha maji shuleni hapo ili kuinusuru shule hiyo
![]() |
| nyumba iliyoshindwa kukamilika kwa wakati |
“Tangu nimefika hapa shuleni kama mwalimu mkuu mwezi Julai
2012, nimeshafunga shule kwa tatizo hili hili, kwa kuwa tunazidiwa” alisema
Katika hatua nyingine mwalimu huyo amesema tatizo hilo la
ukosefu wa maji pia limeathiri ujenzi wa nyumba ya mwalimu shuleni hapo ambapo
ujenzi huo ulikuwa ukamilike Oktoba mwaka jana lakini hadi hivi sasa nyumba
hiyo imefikia sehemu ya linta, na tatizo kubwa ni ukosefu wa maji
![]() |
| Tamali Sanga |
Kwa upande wake Tamali Cyprian Sanga anayesoma darasa la
saba shuleni hapo ambaye pia ni dada mkuu wa shule hiyo amesema tatizo hilo
linawathiri kwa kiasi kikubwa kwani inawallazimu kuosha vyombo vya chakula kwa
kutumia maji ambayo si safi na salama na pia wanakosa vipindi na kwenda kuchota
maji mtoni ama kwenye visima ambavyo vipo mbali na shule
Amesema kuwa vyoo wanavyovitumia kwa hivi sasa ni vichafu na
hakuna maji ya kuvifanyia usafi na pia wanalazimika kuvitumia hivyo hivyo
Kaka mkuu wa shule hiyo Alexanda Marko amesema wakati
mwingine kutokana na uchafu uliokithiri kwenye vyoo hivyo wanafunzi wengine
wanalazimika kurudi makwao kujisaidia huku wengine wakijisaidia kwenye msitu wa
shule hiyo ambao uko jirani na vyoo hivyo hivyo kuwataka wahusika
kulishughulikia ipasavyo tatizo hilo
Shule ya Msingi Ndulamo ina jumla ya wanafunzi 633 ambao
wanategemea maji ili kuendesha shughuli mbalimbali katika shule hiyo
NB:- PICHA ZA VYOO HIVYO NIMESHINDWA KUZIWEKA KWA SABABU YA KIMAADILI


