FISI AMTAFUNA PUA, MIDOMO, MASIKIO


Nhende Ng’wanandilima mkazi wa Kwimba akiwa Hospitali ya Bugando.

Jelard Lucas, Mwanza
AMA kweli pombe mwanaharamu, ukimkuta mtu anasifia pombe basi mpe pole yake kwani hayo ni matumizi mabaya ya akili alizopewa bure na Mwenyezi Mungu, hali imejidhihirisha kwa mkazi mmoja wa Kwimba, Mwanza, Nhende Ng’wanandilima (35) aliyeliwa na fisi sehemu kubwa ya uso wake.

Tukio hilo lilitokea katika Kijiji cha Kibetelwa maeneo ya Nh’ungumalwa, Kwimba ambapo imeelezwa kuwa Nhende alikumbana na kisanga hicho baada ya kunywa ulabu kupita kiasi hivyo kulewa chakari, hali iliyomsababishia kushindwa kujitambua na kuanguka kwenye pori la kijiji hicho na fisi kumkuta.

Kwa mujibu wa mashuhuda, wakati kijana huyo akiliwa, alipiga kelele zilizofika kwenye kijiji hicho ambapo majirani walifika na kumnusuru kisha kukimbiza Hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa matibabu zaidi.

Kwa mujibu wa Nhende, hali aliyonayo kwa sasa inamnyima raha kwani amekuwa kilema, kitu ambacho hakufikiria kinaweza kutokea maishani mwake.
Hata hivyo, alieleza kuwa daktari mashuhuri wa masuala ya koo na mfumo wote wa ‘ogani’ za fahamu amempa matumaini baada ya kumuahidi kumtengeneza upya sehemu zote zilizoliwa na fisi huyo.

“Hali hii si nzuri kwani napata maumivu makali, sikuwahi kujua kama fisi anaweza kumla binadamu hivi, pia namshukuru Mungu nimekatwa nyama za mapaja Jumatatu ya wiki hii ili kusukwa upya kwa mfumo wote wa sura yangu, Dokta Gliyoma ndiyo mkombozi wa maisha yangu.

“Nawashauri vijana wenzangu waache pombe kwani ina madhara makubwa kama niliyoyapata mimi,” alisema.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo