Mwanaume Kilifi alipigwa risasi na kuuawa baada ya kukataa kujisalimisha alipovamia kambi ya jeshi ya Mariakani siku ya Ijumaa, Disemba 9, 2022
Mwanaume huyo mwenye umri wa miaka Juma Kitsao Kombe, alikataa kusikia onyo kutoka kwa mwanajeshi aliyekuwa akilinda lango kuu la kambi hiyo.
Baada ya kugundua kwamba mwanaume huyo hakutaka kutii amri, mwanajeshi huyo aliamua kummiminia risasi na kumuua papo hapo. Kwa mujibu wa ripoti zilizochapishwa na Capital News, mwili wa mwendazake ulitambuliwa na mamake mzazi baada ya kupatikana na polisi, kufuatia tukio hilo.
Inadaiwa kwamba marehemu alikuwa mwanachama wa genge ambalo limekuwa likiwahangaisha wenyeji wanaoishi karibu na kambi hiyo. Kuna madai kwamba Kitsao alifuata ushauri usiofaa kutoka kwa mganga ambaye alimuambia avue nguo zote na kusalia uchi wa mnyama, kabla ya kuvamia kambi hiyo ya kijeshi.
Kitsao alikuwa ameambiwa kwamba akiwa uchi ataweza kumsababisha mlinzi kulala usingizi mzito sana, na hivyo basi ataweza kuiba chochote alichotaka kutoka kwenye kambi hiyo.