Kazi ya uokoaji wa watu waliokuwepo ndani ya ndege ya Precision Air iliyoanguka ndani ya Ziwa Victoria bado inaendelea.
Tayari ndege hiyo imevutwa na sasa ipo karibu zaidi na ufukwe wa Ziwa Victoria.
Hivi punde Mkuu wa mkoa wa Kagera, Albert Chalamila alithibitisha kutolewa kwa miili mitatu katika ajali hiyo iliyotokea mapema hii leo asubuhi.
Akizungumza na waandishi wa habari Mjini Bukoba, Chalamila amesema majeruhi 26 wa ajali hiyo wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Kagera.
Habari zaidi kutoka mkoani Kagera zinaeleza kuwa, muda wowote kuanzia hivi sasa, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwasili mjini Bukoba kuongoza kazi ya uokoaji.
