Mwanamke aliyefahamika kwa jina la Tobanida Mlawa mkazi wa kijiji cha Ikuvilo Kilichopo Kata ya Luhota Wilaya ya Iringa amekutwa amefariki dunia baada ya kujinyonga.
Mashuhuda wa tukio hilo ambao ni wakazi wa kijiji cha ikuvilo wamesema kuwa Tobanida amekutwa amejinyonga chumbani kwake usiku wa kuamkia leo ambapo chanzo cha kifo chake hakijafahamika.
Petro Kisinda ni mwananchi wa kijiji hicho amesema kuwa siku moja kabla ya mama huyo kujinyonga, alimpeleka mwanaye wa kiume kwa babu yake ambapo yeye alibaki nyumbani na mtoto mdogo kabla ya kutekeleza kitendo hicho.
Kwa upande wake MESHACK MLAWA ambaye ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikuvilo amekiri kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema marehemu ,amejinyonga kwa kutumia kamba ya neti.
Amesema kuwa alipokea taarifa hizo saa saba usiku wa kuamkia leo na walishawasiliana na jeshi la polisi kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa tukio hilo.