BAVICHA wafikishwa kwa Pilato huko Dodoma

BAADA ya viongozi wa kitaifa wa Baraza la Vijana wa Chadema (BAVICHA) kusota rumande kwa saa 96 hatimaye leo wamefikishwa mahakamani na kusomewa mashitaka.
Watuhumiwa waliopandishwa kizimbani katika mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma ni Mwenyekiti wa BAVICHA taifa, Patrobas Katambi,
Katibu wa BAVICHA, Julius Mwita, Mwenyekiti wa Bavicha Mkoa wa Mbeya, George Tito na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji BAVICHA taifa, Joseph Kasambala.

Akisoma mashtaka yao mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, James Karayemaha na Wakili wa serikali, Lina Magoma alidai kuwa washtakiwa hao wanashtakiwa kwa kukutwa na maandishi ya uchochezi kinyume na kifungu cha 32 (2) cha Sheria ya Magazeti sura namba 229 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Lina alidai kuwa washtakiwa watatu ambao ni Katambi, Mwita na Tito, mnamo Julai 8 mwaka huu walikutwa katika baa ya Captown mjini hapa wakiwa na fulana zilizoandikwa lugha ya uchochozi.

Wakili wa serikali Lina alinukuu maneno hayo yaliyoandikwa katika fulana hizo kuwa yalikuwa yakisomeka “ Mwalimu
Nyerere: Demokrasia inanyongwa na Dikteta Uchwara”.

Hata hivyo alimsihi hakimu kuwa upelelezi wa kesi hiyo unaendelea na hakuna pingamizi na dhamana inaweza kutolewa kama watoa dhamana watakidhi masariti.

Katika washitakiwa hao Kasambala alifunguliwa jalada lake pekee ambapo shtaka lake linafana na wenzie isipokuwa mahali alipokamatiwa na ujumbe kwenye fulana aliyokuwa ameivaa.

Kwa mujibu wa Wakili wa Serikali Beatrice Nsana, ameeeleza mahakama kwamba Kasambala Julai 9 mwaka huu alikutwa katika kituo cha Polisi cha kati akiwa amevaa fulana yenye maandishi “Mwalimu Nyerere: Demokrasia inanyongwa”.

Washtakiwa wote walikana mashtaka yao ambapo Hakimu Mfawidhi Karayemaha, aliwapa dhamana baada ya kutimiza masharti.

Hata hivyo kesi hiyo imeharishwa na itatajwa tena Julai 26 mwaka huu huku hakiwataadhalisha kutofanya kosa lolote kama hilo na wakifanya watafutiwa dhamana.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo