Siri ya Rais Magufuli na marehemu Sarah Dumba

Rais Dk. John Magufuli, jana amemlilia aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba (pichani), akisema wakati wa uhai wake, alikuwa mtendaji mzuri na hivyo alikuwa katika mpango wa miongoni mwa atakaowateua tena kuendelea na wadhifa huo.
 
Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene, wakati wa maziko ya marehemu Dumba yaliyofanyika katika makaburi ya Magogogoni, Kigamboni wilayani Temeke.
 
Simbachawene aliyemwakilisha Rais Magufuli, alisema kutokana na juhudi zake za kazi, Rais Magufuli aliliingiza jina la Dumba katika orodha ya wakuu wa wilaya watakaoendelea na kazi.
 
“Rais ameshtushwa na kusikitishwa kwa kifo cha Sarah Dumba, alifanya kazi zake kwa uaminifu na juhudi kubwa, jina lake lilikuwa miongoni mwa wakuu wa wilaya wanaotarajiwa kutajwa, lakini mipango ya Mungu hatuwezi kuzuia,” alisema Simbachawene.
 
Aliwataka viongozi wengine kuiga mfano wa marehemu Dumba kwa kufanya kazi bila kuchoka kwa lengo la kuwaletea wananchi maendeleo.
 
Dumba alifariki dunia Jumatatu iliyopita akiwa wilayani Njombe akitekeleza majukumu yake ya kazi. 
 
Katika mazishi hayo, viongozi mbalimbali wa serikali wakiwamo wakuu wa wilaya kutoka sehemu tofauti wakiongozwa na Sofia Mjema, wa Temeke walihudhuria.
 
Wengine waliohudhuria ni viongozi wa dini, vyama vya siasa na wakazi wa Kigamboni.
 

Kabla ya mazishi hayo, ilifanyika ibada ya kumuombea marehemu  katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Usharika wa Magogoni na kuongozwa na Askofu Dk. Alex Malasusa wa Dayosisi ya Mashariki na Pwani.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo