Kituo Kidogo cha Polisi cha Majengo kilichopo katika Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro, kinatumika kuhifadhi mikungu ya ndizi za biashara badala ya kufanya kazi ya
kuwahudumia wananchi.
Hayo yalibainika baada ya baadhi ya wakazi wanaoishi karibu
na kituo hicho ambao hawakutaka majina yao yatajwe gazetini,
kudai kuwa kinatumiwa na mama mmoja mfanyabiashara wa
eneo hilo.
“Tunashindwa kuelewa, hiki ni kituo cha polisi au ni ghala la kuuzia ndizi.
Matukio ya ujambazi
yanafanyika maeneo haya, polisi hatuwaoni na mara chache unaweza kumuona mmoja tena huwa
anapita njia wakati kituo kipo hapa,” alidai mmoja wa wakazi hao.
Akizungumzia madai hayo, jana Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa
alikiri kituo hicho kutumika kinyume cha malengo baada ya kufika na kushuhudia kile
kilichokuwa kikidaiwa na wananchi.
Awali, alisema akiwa njiani akielekea ofisini kwake juzi, alipata taarifa hizo kutoka kwa mwandishi
wa habari mmoja ambaye hakumtaja jina wala chombo chake, ndipo akaamua kuifanyia kazi
taarifa hiyo.
“Nilipigiwa simu na mwandishi akiniuliza juu ya taarifa hizi, nikaamua kwenda moja kwa moja
kituoni hapo lakini tayari nimeshatoa maagizo ya nini kifanyike,” alisema kamanda huyo.
Alisema amewaamuru askari waende kituoni hapo kufanya usafi na kupanga askari watakaokuwa
wakifanya kazi kila siku.
alipoulizwa kuhusiana na kushamiri kwa matukio ya uporaji na ujambazi mkoani hapa, kamanda huyo alisema bado yapo mengi.
Alisena katika mji wa Moshi kwa wiki mbili mfululizo, kumekuwapo na matukio ya ujambazi
lakini kwa sasa yamepungua kutokana na msako mkali waliouanzisha ukiambatana na doria za mchana na usiku zilizosaidia kuwatia mbaroni wahalifu wengi.
chanzo:gazeti la mwananchi