Agizo la kufukua Kaburi huko Geita lazua kasheshe

Amri ya mahakama iliyoruhusu kufukuliwa kaburi lililozikwa mwili wa Samuel Malugala Kikristu, ili uzikwe Kiislamu juzi iliibua mgogoro kati ya familia ya marehemu na waumini wa Kiislamu. 

Wakiongozwa na Imamu wa Msikiti wa Ijumaa, Abdulsalaam Abdallah, uliopo mjini Geita,waumini hao walifika nyumbani kwa marehemu wakitaka kwenda kufukua kaburi hilo, lakini familia ikiongozwa na mdogo wa marehemu, Godfrey Malugara iliwazuia. 

Malugara alidai kuwa mpaka mauti yanamfika, kaka yake alikuwa muumini wa dhehebu la Sabato, hivyo hakuna sababu ya kulazimisha kaburi hilo lifukuliwe na azikwe upya kwa imani nyingine. 

Samuel alifariki dunia Machi 25, mwaka jana akiwa jijini Mwanza na kuzikwa siku iliyofuata kijijini kwake. 

Baada ya juhudi zao kugonga mwamba, waumini hao walifungua shauri mahakamani wakiiomba iwapo haki ya kumzika marehemu na itoe amri ya kufukua kaburi lake. 

Katika maelezo yake, Sheikh Abdallah alisema wenzao waliokuwa wakiishi na marehemu Samuel jijini Mwanza, ndiyo waliowapa taarifa kuwa Samuel alisilimu, madai yaliyopingwa na familia. 

Waumini hao walifika nyumbani kwa marehemu wakiwa na hati waliyodai kuwa ilitolewa na mahakama ikiwaruhusu kufukua kaburi na kumzika upya marehemu kwa imani ya Kiislamu. 

Hatua hiyo ilizua vurugu kiasi cha kusababisha Polisi kuingilia kati kutuliza mzozo huo. Akizungumza nyumbani kwa marehemu baada ya kusoma hati ya mahakama, 

Kamanda wa Polisi Wilaya ya Geita, Ally Kitumbu alidai kuwa hati hiyo ina upungufu kwa sababu haielezi ni nani anapaswa kufukua kaburi na kuwataka waumini hao warudi tena mahakamani wakapatiwe ufafanuzi. 

Baada ya kushauriana, familia na waumini hao walikubaliana kurudi tena mahakamani ili wakapatiwe ufafanuzi zaidi.  


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo