Punda hao walipatikana katika shamba moja karibu mji wa Thika.
Kulingana na wenyeji wa mtaa huo, punda hao walichinjwa na nyama zao kusafirishwa usiku hadi eneo ambalo halijatambulika.
Wakazi wa eneo hilo walipata mizoga ya punda hao siku ya Ijumaa walipokuwa wanapita karibu na shamba hilo.
Joseph Kariuki ambaye ni mkazi wa eneo hilo aliambia Taifa Leo kuwa rafiki yake alikuwa amelalamika kuwa punda wake watatu walikuwa wameibiwa.
“Rafiki yangu alinieleza kuwa punda wake waliibiwa usiku wa kuamkia Ijumaa baada ya kuwafunga kwenye malazi yao,” alisema Bw Kariuki.
Kulingana na wakaazi wengine wa eneo hilo, tukio hilo ni la kwanza kutokea huko.
“Tunahofia kuwa nyama hiyo huenda ikawa imeuziwa watu bila kuangaliwa na daktari kama inavyohitajika,” aliongeza Bw Kariuki.
Wakaazi hao waliomba polisi wa eneo la Thika mjini wawe waangalifu tukio hilo lisitokee siku nyingine.
“Tunahofia kuwa polisi wasipochunguza na kukamata waliofanya kitendo hiki, punda tunaowatumia kubebea watu mizigo wataisha wote,” alisema Bw Peter Njoroge, mkaazi wa eneo hilo.
Polisi walisema kuwa watachunguza tukio hilo mara moja.
