Warioba aibuka kwenye mkutano wa kampeni kumnadi mtoto wake

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba jana aliibukia kwenye kampeni za ubunge, Jimbo la Kawe kumnadi mwanaye, Kippi. 

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Songas, Kata ya Makongo wilayani Kinondoni, Warioba alisema Kippi ni msikivu na asiyependa kuyumbishwa. 

Alisema kama wakazi wa jimbo hilo wanataka mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli afanye kazi kwa ufanisi, basi wampeleke Kippi bungeni kwani anaamini ni kijana mchapakazi. 

“Kippi ni mtoto wangu mkubwa na akiwa nyumbani ni msikivu. Nakumbuka kipindi nafanya shughuli zangu za kisiasa, yeye alikuwa anadandia gari na muda wote alikuwa ni mkimya,” alisema Jaji Warioba ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Kampeni ya CCM. 

Mara kwa mara hotuba yake ilikuwa ikikatishwa na wanachama waliokuwa wakimshangalia, wakati waziri huyo mkuu wa zamani akimnadi Kippi na mgombea udiwani wa kata hiyo, William Iteba. 

Alirejea kueleza kushangazwa na kauli za baadhi ya makada wa zamani wa chama hicho waliohamia Chadema wanaosema miaka 50 hakuna kilichofanyika chini ya utawala wa CCM. 

“Ni ajabu sana hawa wote wanaosema hivi tulikuwa nao huku, na tulishirikiana nao kuleta mafanikio. Niwaambie kitu, kiongozi asiyetambua mafanikio, huyo si kiongozi. Mimi nilipitia huko kama wao, najua haya mambo,” alisema Jaji Warioba bila ya kuwataja waliohamia upinzani. 

Akiomba kura kwa wananchi, Kippi aliwataka wakazi wa Kawe kumpa kura za ndiyo ili awasaidie kutatua kero zao kwa kuwa mwaka huu ni mwafaka wa kuwaletea maendeleo. 

“Nasubiri mnithibitishie Oktoba 25 mwaka huu nianze kazi,” alisema Kippi huku akishangiliwa. 


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo