Kada wa CCM aliyetangaza nia ya kugombea urais kupitia chama hicho wiki iliyopita, Dk. Muzzammili Kalokola, juzi alijionja joto ya jiwe baada ya kupata kipigo kutoka kwa vijana wa ulinzi wa Green Guard wakati akisaka wadhamini mkoani Tanga.
Akisimulia mkasa huo kwa mwandishi kwa njia ya simu jana, alisema , Jumatano baada ya kuwasili nje za ofisi hizo kama alivyotakiwa na Katibu wa wilaya hiyo, ghafla alivamiwa na kundi la Green Guard wakimtaka aondoke.
Alisema walimshambulia kwa kumpiga kisha kumkata mtama na kudondoka, huku Katibu Mwenezi wa Wilaya, akitamka aondolewe katika eneo hilo kwa madai kuwa ‘Mkutano hauwezi kuandaliwa na mwingine halafu mtu mwingine azungumze’.
Tukio la shambulio hilo pia limeonyeshwa katika mitandao mbali mbali ya kijamii, ambapo mtangaza nia huyo alionekana akipigwa na kundi hilo na kuondolewa.
Alisema katibu huyo aliwaeleza vijana hao wamwondoe lakini akiwa eneo hilo la tukio alimpigia simu katibu wa wilaya aliyemtaka awali afike hapo saa 6:00 mchana kuomba udhamini.
“Wakati Katibu wilaya akija eneo la tukio, niliwasiliana pia na Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga (RPC) ambaye awali nilipeleka malalamiko yangu kwake dhidi ya hujuma ninazofanyiwa,” alisema.
Alisema baada ya katibu wa wilaya kufika alimpa simu na kuzungumza na RPC na baadaye alilazimika kwenda polisi na kupewa RB/Tan/58000/2015.
“Kada mwenzangu ndiye anayenichafua, maana nimefika hapa nikavamiwa ghafla halafu jioni saa 12:00 huyo kada alikuja kuomba ridhaa ya wadhamini,” alisema.
Akielezea hujuma alizofanyiwa, Dk. Kalokola alisema baada ya kuchukua fomu Dodoma alipewa barua za utambulisho kwa kila katibu wa mkoa ili wakasaini daftari la wageni na hatua nyingine zifuate.
