HOTELI ya JB Belmont ambayo viongozi wa kitaifa na kimataifa hufikia imefungwa kutokana na kushindwa kutimiza masharti ya mkataba kati yake na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Akizungumza na MwanaHALISI online kwa njia ya simu, Meneja wa NSSF Kanda ya Ziwa, Hamis Fakhi alikiri hoteli hiyo kufungwa huku akishindwa kubainisha sababu ambapo aliahidi kuzungumza na waandishi wa habari kesho.
“Ni kweli tumefunga hoteli hiyo lakini sina maelezo mengine zaidi ya hayo, kwani hata makubaliano ya mkataba kati ya mmiliki wa hoteli na NSSF yalifanyika Makao Makuu,” amesema.
Hata hivyo, hajafahamika kama kulikuwa na wateja ndani ya hoteli hiyo kwa kuwa, hakuna mtu aliyeruhusiwa kuingia ndani kutokana na kuwepo kwa tangazo hilo huku eneo la mbele ya hoteli likiwa limezungushiwa kamba.
Hoteli hiyo ambayo ilikuwa ikimilikiwa na Raia wa Uganda, Justus Buguma ambaye sasa ni marehemu.
Kabla ya kubadilishwa jina na kuitwa JB Belmont, ilikuwa ikijulikana kwa jina la Nyumbani Hoteli ikimilikiwa na aliyewahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Vunjo (CCM), Aloyce Kimaro ambaye naye inadaiwa aliondolewa na NSSF ndani ya jengo hilo baada ya kushindwa kulipa kodi.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa, baada ya marehemu Bugumba kufariki Februari 13, 2013, hoteli hiyo hivi sasa inamilikiwa na familia yake ambapo tena imekumbana na kisa kile kile kilichomkuta Kimaro.
chanzo:mwanahalisionline
