CCM MBEYA YAVUNA VIJANA 79 WA CHADEMA


ZAIDI ya vijana 79 waliokuwa wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Kata ya Nzovwe, mkoani Mbeya, wamekihama chama hicho na kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
 
Mbali ya kupewa kadi za CCM, vijana hao walidai kuchoshwa na sera za CHADEMA zinazohamasisha maandamano badala ya kuwajengea uwezo kiuchumi ili waweze kujikomboa kimaisha.
 
Vijana walipokelewa na Mjumbe wa Mkutano Mkuu Taifa jijini humo, Bw. Charles Mwakipesile, kufungua tawi lao la wateule Nzovwe ambapo vijana hao walidai wamejipanga kukijenga chama hicho, kulinda amani na kujijenga kiuchumi.
 
Awali, Katibu wa vijana hao, Bw. Simon Charles, alisema vijana wengi waliopo CHADEMA, wamekuwa wakitumika kuwanufaisha wanasiasa kwa kushiriki maandamano ambapo mwisho wa siku, hupata ulemavu wa kudumu au kupoteza maisha.
 
"Kwa kutambua ukweli huu, tunaamini mustakabali wa maendeleo ya Watanzania, bado uko mikononi mwa CCM ndio maana tumeamua kurudi kundini tukiwa na malengo kudumisha amani, kujenga mshikamano thabiti ndani ya chama," walisema.
 
Akizungumza baada ya kufungua tawi hilo, mgeni rasmi Bw. Mwakipesile, alisema hatua waliyochukua vijana inapaswa kuigwa na vijana wengine waliopo CHADEMA.
 
Alisema umefika wakati wa vijana kukataa siasa zenye mrengo wa chuki ambazo hazisaidii kuwatoa katika lindi la umaskini ambapo chama tawala CCM, kinafanya kazi kubwa ya kusimamia ilani yake ya uchaguzi, kudumisha amani na utulivu nchini.
 
"Lazima tujitafakari na kupinga vikali kauli za wanasiasa ambao wanahamasisha maandamano lakini vijana ndio wanaoumia ambapo wao wanapanda ndege na kwenda kupumzika Ulaya.
 
"Huu ni unyama ambao lazima muukatae na kudumisha amani iliyopo ambayo ndiyo matunda ya uhuru tulioupata...nawaomba Watanzania muunge mkono juhudi zinazofanywa na Rais Jakaya Kikwete za kuleta maendeleo na kudumisha demokrasia miongoni mwa wananchi," alisema.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo