AJALI YAUA MAHABUSU WANNE NA ASKARI HUKO MKURANGA PWANI

 Picha na maktaba.

Mahabusu  wanne na askari Magereza, Sajenti Peter Mabuma, wamefariki dunia baada ya gari walilokuwa wamepanda kugongana na lori na kupinduka katika Wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani.

Wakati mahabusu na askari hao wakikumbwa na masaibu hayo, idadi ya abiria waliokufa kutokana na ajali ya basi la Kampuni ya Luhuye, iliyotokea juzi, katika Kijiji cha Yitwimila, Wilaya ya Busega, mkoani  Simiyu, imeongezeka kutoka 12 hadi 17 baada ya majeruhi watano kufariki asubuhi katika hospitali ya Rufaa Bugando, mkoani Mwanza.

Mahabusu waliofariki dunia wametajwa kuwa ni Juma Mohamed (19), Faraja Msahamu (40), Alex Athumani (23) na Hamis Juma (38).

Askari Magereza aliyefariki dunia alikuwa akiwasindikiza mahabusu hao kutoka katika Mahakama ya Mwanzo Kimanzichana, kuwapeleka katika gereza la Keko, jijini Dar es Salaam.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Ulrichi Matei, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo jana, majira ya saa 6.00 mchana.

Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya gari lililokuwa limewabeba mahabusu hao, ambalo ni mali ya Jeshi la Magereza, lenye namba za usajili MT 0038, kuligonga lori hilo na kupinduka. 

Gari lililowabeba mahabusu lilikuwa likiendeshwa na Koplo Zawadi Makupa (41). Lilikuwa likitokea katika Mahakama ya Kimanzichana.

Kamanda Matei alisema lori hilo lenye namba za usajili T446 CJS lilikumbwa na mkasa huo wakati likiwa limeegeshwa pembezoni mwa barabara katika Kijiji cha Kinene Mwalusembe, wilayani humo.

Alisema mahabusu wote pamoja na askari huyo walifariki dunia katika eneo la tukio na miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mkuranga.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya hiyo, Francis Mwanisi, alithibitisha maiti kuhifadhiwa katika hospitali hiyo na kwamba, hali ya askari aliyejeruhiwa katika ajali hiyo ni mbaya.

Alisema askari huyo amepata majeraha makubwa kichwani na kwenye mikono yote miwili na kwamba, kwa hali hiyo wamepanga kumhamishia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), jijini Dar es Salaam.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo