Kutokana na uwepo wa mvua nyingi katika wilaya ya Makete msimu huu wa masika, hali hiyo inapelekea baadhi ya maeneo katika barabara, maji kupita juu ya barabara ama maji hayo kukusanyika eneo moja na kushindwa kutembea
Hali hiyo inasababishwa na kuziba kwa mifereji ya kupitishia maji kandokando mwa barabara kutokana na shughuli za kibinadamu ikiwemo kukata miti na matawi yake kuachwa kwenye mifereji ya barabara, kutupa taka ovyo kwenye mifereji ya maji pamoja na kutofanyiwa uangalizi wa mara kwa mara wa barabara endapo mitaro hiyo inaziba
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa eddy blog ambaye ametembea maeneo kadhaa ya barabara ya Makete - Njombe ameshuhudia kuziba kwa mitaro hiyo ambapo maji yakishindwa kupita hutapakaa juu ya barabara na hatimaye maji hayo huaribu barabara pole pole
Akiwa eneo la Tandala mwandishi wetu alishuhudia takataka zikiwa zimeziba kalavati la kupitishia maji kutokana na watu kutupa taka ovyo pamoja na taka nyingine zinazoletwa na maji ya mvua hivyo kutokana na kukosekana kwa uangalizi wa wahusika kuzibua eneo hilo maji hulazimika kupita juu ya barabara na kujitafutia mkondo usio sahihi wa kupitisha maji hayo
Hali ya maji ya mvua kuharibu barabara eneo hilo pia imesababishwa na kuziba kwa mifereji ya kupitishia maji kulikosababishwa na kuota kwa nyasi ndefu pamoja na udongo hali inayosababisha maji kukosa mwelekeo
Kwa upande wa Makete mjini pia hali ipo hivyo hivyo ambapo kwa kiasi kikubwa mifereji imeziba na mingine haina uelekeo wa kupeleka maji, hivyo maji mengi huzagaa barabarani
Aidha mtandao huu unashauri ngazi husika kuliangalia suala hili kwa makini kwa kuwa mambo huanza kidogo kidogo lakini mwisho wa siku fedha au gharama nyingi hutumika kwa ajili ya kufanya matengenezo ambayo yangweza kuzuilika
imeandaliwa na mwandishi wetu Edwin Moshi.



