Wazee hao wanasemawamelazimika
kuchukua hatua hiyo baada ya serikali kushindwakumaliza visa vya watu
wenye mvi kuuawa kikatili na watu wasiojulikana kwa kudaiwa kuwa
wachawi.
Walisema hawana budi kujitetea dhidi ya kushabuliwa na kuuawa na genge linalolenga wazee wenye mvi na macho mekundu.
Wanadai kuwa idadi ya wazee imepungua kutokana na mauaji hayo na wanajaribu kuepuka mauti.
“Mimi nimeamua kunyoa nywele niwe na
kipara kwa sababu naogopa kuuawa. Wajua wazee na watu wenye mvi
wanauawa kiholela. Hofu imetanda katika kaunti hii kufuatia visa hivyo.
Na si mimi peke yangu; wenzangu wengi wananyoa kwa kuwa tunatahadhari
kabla ya hatari” akasema mzee mmoja aliyehojiwa na Taifa Leo.
Visa vya mauaji ya watu wenye mvi
ama wazee vimeongezeka eneo la Pwani huku wakazi wakitoa wito kwa
serikali kuthibiti usalama na kuwachukulia hatua kali wanaotekeleza
mauaji hayo.
Katika Kaunti ya Kilifi, wazee wanne wameuawa kwa kushukiwa kuwa wachawi katika maeneo ya Vitengeni na Pinglikani.
Visa hivyo vimewafanya wakazi waamue kunyoa nywele zao ili kuficha mvi ambazo zinawafanya wadhaniwe kuwa wachawi.
“Mvi si ishara ya heshima tena;
imekuwa ishara ya mauti na tunaogopa kumea mvi kwa kuwa wakati wowote
utauawa. Tunaomba msaada la sivyo sisi wazee tutamalizwa,” akasema Bi
Karisa Kadzo, akiwa mafichoni baada ya kuonywa kwamba atauawa kwa madai
anajihusisha na uchawi.
Ajuza huyo alisema yeye ni mcha
Mungu na hajawahi kujihusisha na uchawi. Aliwataka viongozi wa eneo hilo
wajitokeze na kuhamasisha vijana dhidi ya maovu hayo akisema adhabu
yake ni kali sana mbele ya Mungu.
“Tumeishi kwa miaka na mikaka na
kamwe hatujawahi kushukiwa kuwa wachawi. Ikifika mahali mtu anatoroka
kwake na kwenda mafichoni ujue hali ni mbaya. Hiki kizazi cha sasa
hatujui kimetoka wapi? Tunatoa wito kwa viongozi wachukue hatua
madhubuti,” akasema huku akidondokwa na machozi.
Katika kipindi cha wiki moja tu,
wazee wanne wameuawa kwa kushukiwa kuwa wachawi. Jumatatu iliyopita,
katika eneo la Pingilikani, Chonyi, mzee wa miaka 65 kwa mikuki kisha
akachomwa moto.
Kasena Mwakamusha Baya aliuawa baada
ya kutoka eneo la Kwale ambako inasemekana alikuwa ameenda kulishwa
kiapobaada ya kushukiwa kuwa mchawi.
Kulingana na itikadi za Wamijikenda,
mtu anaposhukiwa kuwa mchawi hulishwa kiapo kumzuia kuendeleza uchawi.
Inasemekana mshukiwa pia huanza kufanya mambo kinyume cha alivyokuwa
kabla ya kiapo hicho.
Walioshuhudia walidai kuwa marehemu
alianza kufura mashavu ndipo vijana wakamrukia kwa mikuki na ngumi kabla
ya kumtia moto.Afisa mkuu wa polisi wa eneo hilo, Justine Nyagah,
alithibitisha kuwepo kwa uhalifu huo na kutaja kuongezeka kwa mauaji ya
aina hiyo.
Uchunguzi
“Punde mtu anapoota mvi anaanza
kushukiwa kuwa mchawi. Hii ni dhana potovu miongoni mwa wakazi.
Ninawatahadharisha kuwa tutachukua hatua madhubuti,” akasema huku
akisisitiza kuwa wameanzisha hamasisho dhidi ya hulka hiyo.
Maeneo mengine ambapo watu wameuwawa
wiki hii ni Jaribuni na Dera. Huku hayo yakijiri, maafisa wa polisi
katika wilaya ya Changamwe wameanzisha msako dhidi ya genge la vijana
lililoshambulia familia moja katika nyumba yao kabla ya kuwateketeza
hadi kufa katika eneo la Miritini wilayani humo. Akiongea na Taifa Leo
kwa njia ya simu, afisa mkuu wilayani humo Joseph Muthee, alisema
polisi wameanzisha uchunguzi dhidi ya mauaji hayo ya kikatili.
“Watu wawili walichomwa ndani ya
nyumba yao kwa kushukiwa kuwa wachawi jana usiku. Tumeanzisha uchunguzi
tukilisaka genge hilo ambalo limeanza kushambulia watu kwenye majumba
yao” alisema Bw Muthee. Naye kaimu chifu wa eneo hilo, Matano Hassan,
alithibitisha kuwa wawili hao walikuwa mke na mumewe na waliteketezwa na
vijana kwa njia ya kikatili kwa kushukiwa kuwa wachawi.
“Hii familia ya watu wa mawaku
walikuwa wakijishughulisha na kilimo na kujitafutia riziki lakini ni
masikitiko na mshangao mkubwa kwa watu kuwashambulia nyumbani kwao,
kuwaburura hadi nje, kuwafunga kwa kamba kabla ya kuwateketeza; ni
unyama na udhalimu” akasema kaimu huyo.
Bw Matano alisema kuwa wawili hao
ambao walikuwa wanaishi peke yao walikuwa wazazi wa watoto wawili.
“Walikuwa wazazi wa watoto wawili japo watoto wao walishahama.
Tutawakamata wale wote waliohusika” akahakikishia umma.
“Dadaye mume ametuarifu kuwa wawili
hao walikuwa watu wakarimu, wacha Mungu na wamepigwa na butwaa kusikia
wamechomwa” akasema huku akionya umma dhidi ya kuchukua sheria mikononi
mwao.
Na wakazi wa eneo la Kisauni
wamepigwa na butwaa baada ya mtoto wa miaka mitatu kupatikana katika
kichaka akitoa povu kinywani. Kulingana na afisa wa mitaa eneo la
Kisauni, Abdhallah Abdhulrahman, mtoto huyo alipewa sumu na kutupwa
msituni.
“Tulijulisha polisi na tukampeleka
hospitali kuu ya mkoa lakini alifariki alipokuwa akitibiwa. Wazazi wake
hawajulikani,” akasema Abdhallah.