BAJETI YA BILIONI 2.5 YASABABISHA RAIS UHURU KENYATTA KUVUNJA KAMATI YA MIAKA 50 YA UHURU

 Uhuru Kenyatta
Na Peter Mwai.
RAIS Uhuru Kenyatta amevunjilia mbali kamati iliyokuwa imeundwa kuandaa maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru baada ya kamati hiyo kupendekeza bajeti ya Sh2.5 bilioni.
Taarifa iliyotumwa na msemaji wa Ikulu, Manoah Esipisu ilisema Rais anafahamu kuwa kamati hiyo ilitayarisha bajeti ya Sh2.5 bilioni na kusema haiambatani na mipango ya serikali ya Jubilee ya kutumia vyema fedha na rasilimali za umma.

“Kwa kupendekeza kiasi kikubwa hivyo cha pesa kutumiwa kwa maadhimisho, kamati hiyo ilionyesha wazi kwamba haielewi mtazamo wa kifedha ulioko kwenye serikali,” alisema.

“Kutokana na hayo, Rais Kenyatta ameagiza ivunjiliwe mbali.”
Kamati hiyo ilikuwa ikiongozwa na Katibu wa Wizara ya Usalama Mutea Iringo.

Rais Kenyatta alisema ingawa sherehe hizo ni muhimu sana kwa taifa, zinatokea wakati ambao serikali inaangazia zaidi utumizi mwema wa fedha za umma ikizingatiwa hali ngumu ya kiuchumi iliyopo.

Ikulu
Kamati mpya itaundwa na itahusisha sana maafisa kutoka kwa Wizara ya Michezo, Utamaduni na Sanaa ambayo alisema ina utaalamu sana kuhusu mambo kama hayo.

Aidha, itakuwa pia na wadau wengine wakiwemo watu kutoka sekta ya kibinafsi. Ikulu binafsi itafuatilia shughuli za kamati hiyo mpya.

Habari kuhusu bajeti hiyo ambayo iliwagadhabisha Wakenya wengi, ilifichuliwa na gazeti la Nation. Kamati hiyo ilikuwa imependeza Sh50 milioni zitumike kutengeneza sanamu ya shaba ya Rais mstaafu Mwai Kibaki akishikilia katiba.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo