Watu wanne
wamejeruhiwa mmoja wapo vibaya sana kufuatia dereva aliyekuwa akijifunza
kuendesha gari kwenda kuparamia watu waliokuwa katika baa ya pombe za
kienyeji inayojulikana kwa jina la Ukumi iliyopo katika eneo la Usagara
jijini Tanga.
Waliojeruhiwa
katika ajali hiyo ni mzee Ally Kangajaka mwenye umri wa miaka 68,Juma
Sabas Baharia wa mamlaka ya bandari Tanga, Millian Mngazija mama lishe
na Godfrey Msagati ambaye amejeruhiwa vibaya sehemu za kichwani ambapo
wote wamelazwa katika hospitali ya rufaa mkoani Tanga wanaendelea na
matibabu.
Wakielezea
tukio baadhi ya mashuhuda wamesema dereva aliyejulikana kwa jina la
Juma Mwinzari alichukua gari la mmiliki anayejulikana kwa jina la Mussa
Shemkhai na kuliendesha ndipo lilipomzidi nguvu na kwenda kuparamia watu
waliokuwa katika kilabu cha pombe za kienyeji cha Ukumi kisha kugonga
ukuta.
Kwa
mujibu wa mashuhuda waliokuwa katika eneo la tukio wamedai kuwa baada
ya ajali hiyo mmiliki wa gari alikuwa akijiandaa kuliondosha gari hilo
kabla askari hawajafika ndipo alipokutana na baadi ya vijana waliotaka
kumpiga wakimtaka aliache gari hilo hadi askari watakapopima kwa mujibu
wa sharia.
Kufuatia tukio hilo jeshi la polisi linawashikilia watu
wawili, mmiliki wa gari hilo na mtuhumiwa ili sheria iweze kuchukua
mkondo wake.
ITV