Halmashauri ya wilaya ya Makete
imeshindwa kufikia lengo lake la kufikia makisio ya mapato ya ndani ya shilingi
276, 340,000 katika kipindi cha Januari – Aprili 2013, na badala lake
imefanikiwa kukusanya milioni 104 ndani ya kipindi hicho
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa
wilaya ya Makete ya Makete Mh. Josephine Matiro wakati akiwasilisha taarifa ya
utekelezaji wa shughuli za serikali katika wilaya yake kwa kipindi cha
Januari-Aprili mwaka huu
Mkuu huyo ametaja sababu
zilizopelekea halmashauri kutofikia lengo lake la kukusanya mapato hayo kuwa ni
pamoja na uharibifu wa miundombinu ikiwemo barabara nyingi kutopitika kutokana
na mvua zilizonyesha wilayani mwake, hali ya hewa kutoruhusu pamoja na
wafanyabiashara wengi kusitisha biashara zao ikiwemo mbao na viazi kutokana na
maeneo mengi kutofikika
“baadhi ya wafanyabiashara
walisitisha kufanya biashara zao kama mbao na viazi kutokana na maeneo
wanayofanyabiashara kutofikika kiurahisi” alisema Matiro
Amesema kutokana na halmashauri
kutofikia malengo hayo baadhi ya barabara zitakarabatiwa msimu huu ili zipitike
na kufikia maeneo yote waliyoshindwa kuyafikia pamoja na kuongea na wakala wa
barabara Tanroads mkoa wa Njombe kukarabati pia barabara zile zilizopo chini
yao
Mkuu huyo wa wilaya amejiwekea
utaratibu wa kutoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli za serikali kila baada ya
miezi mitatu ambapo huitoa kwa wananchi wote wa wilaya yake ambapo katika
taarifa hiyo hujumuisha sekta zote ikiwemo kilimo, afya, maji, elimu,barabara,
maliasili na utalii