Waziri wa elimu
sayansi na teknolojia Prof Joyce Ndalichako ameonesha kutoridhishwa kwake na
ujenzi wa mabweni na nyumba za walimu katika chuo cha ufundi VETA Makete baada
ya kufanya ziara chuoni hapo hii leo
Waziri Ndalichako
amesema mkandarasi anayejenga majengo hayo ambaye ni wakala wa Majengo nchini
(TBA) analeta masihara na kazi ya serikali ya awamu ya 5, ambapo tangu
akabidhiwe kazi hiyo Oktoba Mwaka jana hii leo ndio ameanza kazi ya kusafisha
uwanja kwa ajili ya ujenzi huo
Akipatiwa maelezo ya
mradi huo ambayo hayakumridhisha kutoka kwa Mkandarasi huyo, waziri Ndalichako
amesema kwa sasa hana imani na TBA kutokana na kuonesha kukwamisha kazi
alizopewa na serikali katika maeneo tofauti hapa nchini
Waziri Ndalichako
ametilia shaka gharama zitakazotumika kujenga nyumba za walimu ambapo nyumba
moja inatarajiwa kujengwa kwa zaidi ya shilingi milioni 160 jambo ambalo
amesema ni gharama kubwa kuliko serikali inavyotaka
“Sisi wizara ya elimu
tumekuwa tukijenga nyumba za walimu kwenye shule mbalimbali hapa nchini kwa
kati ya shilingi milioni 60 hadi 70, sasa iweje hapa iwe milioni 165, mbona
mnajenga nyumba za kifisadi?” amesema Ndalichako
Pia ameshangazwa na
taarifa inayoainisha kuwa gharama ya ujenzi wa bweni moja la kubeba wanafunzi
40 utagharimu zaidi ya shilingi milioni 300 na kusema hayuko tayari kutoa fedha
hizo kwa kuwa ni kubwa kupita kiasi
Amesema wizara yake
ina fedha nyingi kwa ajili ya kuhakikisha sekta ya elimu inaboreshwa hivyo
hakuna kisingizio cha kukosa fedha
“Meneja wa kanda,
kama mtajenga bweni kwa fedha hii nakuhakikishia huna kazi, hii fedha ni nyingi
mno” amesema Waziri
Hata hivyo mkandarasi huyo amemuomba na kumhakikishia waziri kuwa atajitahidi ujenzi huo ukamilike kabla ya muda uliopangwa, hivyo waziri amuamini kwa hilo, jambo ambalo Mh Ndalichako amelitilia shaka na kusema hana imani na TBA na wakitaka imani yake irejee waifanye hiyo kazi kwa vitendo
Katika hatua nyingine
waziri huyo amekagua majengo ya chuo hicho na kuridhishwa na ujenzi wake wa
kiwango, ambapo amesema licha ya mkandarasi aliyejenga majengo hayo kusimamishwa
kwa kukiuka sheria ya manunuzi, lakini alijenga vizuri na kusema anastahili
kurudishwa na aendelee na kazi, kwa kuwa anatambua thamani ya fedha ya serikali
“Ni afadhali huyu
aliyejenga haya majengo ya VETA karibia 8 na ameyajenga kwa kiwango halafu
amesimamishwa kwa kukiuka taratibu za manunuzi, lakini ni bora huyu anayekiuka
taratibu za manunuzi lakini kajenga majengo mazuri kuliko hawa wanaotaka
kujenga kwa gharama kubwa halafu wanasuasua, mimi naagiza arudishwe
Mkandarasi huyo akieleza jambo kwenye ziara hiyo ya Waziri Prof Joyce Ndalichako
Waziri wa elimu Prof Ndalichako (kulia) akikagua eneo linapojengwa nyumba za walimu wa chuo cha VETA Makete
Mtambo ukiendelea kusafisha eneo la ujenzi wa Mabweni ya wanafunzi Chuo cha VETA Makete
Waziri Ndalichako akimtahadharisha Mkandarasi wa ujenzi huo
Ukaguzi wa waziri Ndalichako ukiendelea