Moto waharibu kampeni za CHADEMA Makete

Na Eddy Blog, Makete.

Wakazi wa vitongoji vya Luchala, Uchewa, Posta na vya jirani wamelazimika kuacha shughuli zao za kila siku na kuzima moto uliozuka ghafla katika kitongoji cha Uchewa kata ya Tandala wilayani Makete

Moto huo unadaiwa kuzuka jana majira ya saa 6 mchana ambapo umeunguza mashamba ya miti iliyokuwa katika kitongoji hicho, ambapo jitihada za wananchi hao kwa pamoja zimesaidia kuuzima moto huo pamoja na kunusuru mashamba mengine yasiteketee kwa moto huo

Wananchi hao wake kwa waume wameonekana na mwandishi wetu wakishughulika kuuzima moto huo kwa matawi ya miti, kuondoa nyasi katika maeneo ambayo moto huo haujafika pamoja na kuchota maji ambayo pia yametumika kuuzuia moto huo usisambae zaidi

Baadhi ya wananchi tuliozungumza nao huku wakiendelea kuzima moto huo wamesema huu sio muda wa kumtafuta aliyesababisha moto huo, bali ni muda wa kuhakikisha moto huo unazimwa na kuudhibiti usiende mbali zaidi jambo ambalo wamefanikiwa kulifanya na hivyo baadaye watamtafuta aliyesababisha moto huo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake

Katika hatua nyingine tukio hilo limesababisha zoezi la uzinduzi wa kampeni za chama cha demokrasia na maendeleo CHADEMA ngazi ya kata ya Tandala kuahirishwa kwa muda kutokana na moto huo, kwani viongozi pamoja na wafuasi wao waliamua kwenda kushiriki kuuzima moto huo

Kampeni hizo zilikuwa za kumnadi mgombea udiwani wa kata hiyo kupitia CHADEMA Bw. Artin Sanga ambapo amewaasa wakulima ambao wakati huu wanaandaa mashamba yao kwa ajili ya msimu ujao wa kilimo kuwa makini na moto wanaowasha ili usilete madhara kama hayo na baada ya kufanikiwa kuudhibiti moto huo ndipo waliondoka na kuelekea eneo la mkutano wa kampeni kama walivyokuwa wamepanga


Hadi mwandishi wetu anaondoka eneo la tukio haikufahamika mara moja nini chanzo cha moto huo wala mhusika au wahusika waliosababisha
 Jitihada za kuzima moto zikiendelea
 Wananchi wakishiriki pamoja kuuzima moto huo
 Mkazi mmoja wa kitongoji cha Uchewa akishukuru baada ya moto huo kuzimwa


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo