
MAHAKAMA moja mjini Naivasha imemhukumu mwanamke mwenye umri wa miaka 34, miaka mitano gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kummwagia mwanamke mwingine supu moto.
Maria Waruhi
alifikishwa mbele ya hakimu mkazi wa Naivasha, Bi Selina Muchungi na
kushtakiwa kwamba mnamo Mei 19, 2012 katika mtaa wa Kabati, mjini
Naivasha, alimmwagia mchuzi moto Bi Mary Wanjiku na kumjeruhi vibaya.
Mahakama
iliambiwa kwamba Bi Wanjiku alikuwa ameenda sokoni ambako alikuwa akiuza
matunda. Alipofika kibandani mwake, mshtakiwa alimmwagia supu hiyo ya
githeri.
Mashahidi
aidha walisema kwamba kabla ya kisa hicho, wawili hao walikuwa
wamegombana baada ya Bi Wanjiku kumuuliza Bi Waruhi kwa nini alikuwa
amemwaga supu katika kibanda chake.
Akisaidiwa na wanawake wengine sokoni humo, Bi Wanjiku aliripoti kisa hicho kwa polisi ambao walimkamata mshtakiwa.
Bi Wanjiku alitibiwa katika Hospitali ya Naivasha na kuruhusiwa kwenda nyumbani.
Akitangaza uamuzi huo, Bi Muchungi alikikashifu kisa hicho ambacho alikitaja kama kosa linalohitaji adhabu kali.