Watu watano wameripotiwa kufariki dunia baada ya jengo la ghorofa walilokuwa wanajenga kuanguka katika eneo la Marangu Sembeti wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro.
Taarifa zinasema tayari kikosi cha uokoaji kimefika eneo hilo kwa ajili ya kuwaokoa watu wengine wanaosadikiwa kufunikwa na jengo hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro Simon Maigwa, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo.
Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Kamanda wa Jeshi la zimamoto na uokoaji mkoani hapa, Jeremiah Mkomagi amesema ghorofa hilo lilikuwa likiendelea kujengwa na taarifa walizozipata kulikuwa na mafundi na vibarua wapatao 30.
Amesema ghorofa hilo lilianguka Desemba 18 usiku wa saa mbili kuelekea saa tatu wakati mafundi na vibarua hao wakiendelea na kazi ya kumimina zege.
"Uchunguzi wa awali unaonesha jengo lilijengwa ndani ya muda mfupi na halikufuata utaratibu wa ujenzi na nondo zilizotumika ziko chini ya kiwango," amesema Kamanda Mkomagi