Mshukiwa amuua mpenzi wake, apiga simu polisi

Polisi wanamsaka mshukiwa aliyemuua mpenziwe na kupiga simu katika kituo cha polisi cha Isinya kaunti ya Kajiado nchini Kenya kuripoti kisa hicho.

Mshukiwa aliambia polisi kwamba alimuua mwanamke huyo mnamo Februari 3.

Kulingana na polisi, mshukiwa, mwenye umri wa miaka 27, alifahamisha polisi kwamba alimuua mpenzi wake aliyetambulika kama Risper Ngendo Munene, 24, katika nyumba ambayo alifanya kazi kama mlezi katika lokesheni ndogo ya Olooltepes, eneo la Oloosirkon kaunti ndogo ya Isinya.

Polisi walisema mshukiwa huyo kisha akakata simu na kutoweka. Simu yake ya rununu imezimwa tangu wakati huo.

Maafisa hao wa usalama walizuru eneo la tukio wikendi na kupata mwili wa Ngendo ndani ya nyumba, ambayo ilikuwa imefungwa.

Mwili ulikuwa umefunikwa na blanketi kitandani na alama nyeusi kwenye viungo na shingo na ulikuwa umevimba. 

Mwanamke huyo alikuwa amesafiri hadi eneo hilo kumtembelea mwanamume huyo wakati kisa hicho kilipotokea.

Mwili ulioharibika ulihamishwa hadi Nairobi Funeral Home (City Mortuary) ukisubiri kufanyiwa uchunguzi.

Polisi walisema bado hawajabaini sababu za mauaji hayo.  Msako wa mshukiwa unaendelea, polisi walisema.

Huku hayo yakijiri, polisi wanachunguza kisa ambapo mshukiwa wa mauaji alipatikana akiwa amefariki katika seli katika kituo cha polisi cha Chogoria, Kaunti ya Tharaka Nithi.

Mshukiwa pia alikuwa anazuiliwa katika kituo hicho kwa madai ya utekaji nyara wa watoto. James Muthaura, 30, alipatikana amefariki Alhamisi asubuhi, polisi walisema.

Polisi katika kituo hicho walisema washukiwa wengine waliokuwa wakizuiliwa hapo walipiga kelele ili wasikilizwe, na walipochunguza, walikuta mtu huyo amefariki dunia kwa kujitoa uhai huku akijinyonga kwenye sehemu ya kutolea hewa.

Inasemekana Muthaura alitumia nguo yake ya ndani kujinyonga. Nguo hiyo ya ndani ilikutwa imefungwa shingoni.

Maafisa wakuu wa polisi walitembelea eneo la tukio kama sehemu ya uchunguzi wa tukio hilo.

Maafisa hao wamealika Mamlaka Huru ya Uangalizi wa Polisi kujiunga katika uchunguzi huo. Mwili huo ulihamishiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Rufaa ya Chuka ukisubiri kufanyiwa uchunguzi.

Katika kituo cha polisi cha Laisamis, washukiwa wawili wa kiume walitoroka kutoka kizuizini katika hali isiyoeleweka.

Wawili hao waliotambuliwa kama Abraham Kimeto na Peter Gitau walikuwa wamezuiliwa kwa kuvunja na kuiba na kushughulikia mali iliyoibwa walipotoroka Alhamisi asubuhi.

Walipangwa kufika mbele ya mahakama inayotembea katika eneo hilo wakati kisa hicho kilipotokea.

Polisi walisema waliwapata wakiwa hawapo na inashukiwa waliwezeshwa kuondoka.

Afisa wa polisi ambaye alikuwa zamu wakati huo alikamatwa kama sehemu ya uchunguzi wa tukio hilo, polisi walisema.

Msako unaendelea katika eneo hilo ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwakamata washukiwa hao.

Chanzo:Radio Jambo


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo