Injinia ashushwa cheo kutokana na Utendaji Mbovu

Charles Kuyeko, Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala (aliyesimama).
INJINIA Japhary Bwigane, Kaimu Mhandisi Mkuu Kitengo cha Ujenzi katika Manispaa ya Ilala ameshushwa cheo na Kamati ya Fedha ya Utawala ya Baraza la Madiwani la manispaa hiyo kutokana na utendaji mbovu

Watumishi wengine wa kitengo hicho waliowajibishwa kwa kushushwa vyeo ni Injiania Siyajali Mahili na Daniel Kirigiti ambao ni wasaidizi wa mkuu huyo.
Watumishi hao wanatuhumiwa kwa usimamizi mbovu wa miradi mbalimbali chini ya kitengo hicho na kwamba, kitengo hicho kimekuwa kikituhumiwa kufanya kazi kinyume cha taratibu.

Charles Kuyeko, Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala pia Diwani wa Bonyokwa (Chadema) akizungumzia hatua hiyo amesema, watumishi hao walipewa kazi ya kusimamia ujenzi wa baadhi ya barabara zilizomo wilayani humo ikiwemo ya Tabata St. Marry’s.

Akitoa mfano wa barabara ya Tabata-St. Marry’s amesema, haina ubora uliotakiwa na kwamba, kwa mujibu wa makubaliano wanapaswa kuirudia kwa gharama za kampuni iliyotengeneza.

Kuyeko amesema, watumishi hao hawana ushirikiano na madiwani wa maeneo ya barabara zenye matatizo ambazo walikuwa wakisimamia na kuwa, hata walipoitwa kuelezwa matatizo ya wananchi, wamekuwa wakaidi.

“Kwa hivyo, kufuatia ukaidi wa mainjinia hao kwa madiwani, Balaza la Madiwani lililokaa Jumamosi ya wiki iliyopita na Jumatatu wiki hii liliazimia kuwashusha vyeo watu hao ili iwe fundisho kwa wengine watakaoteuliwa,” amesema Kuyeko na kuongeza kwamba, uchunguzi unaendelea.

Kuyeko ametoa tahadhari kwa watendaji waliopo katika wilaya hiyo kuwa, wanapaswa kubadilika na kutambua kuwa, huu ni utawala mpya ambao upo kwa ajili ya kuwasaidia wananchi na si vinginevyo.

Akizungumzia hatua za maendeleo katika Wilaya ya Ilala Kuyeko amesema, tayari ujenzi wa madarasa katika kila shule yenye uhitaji umeanza ambapo wanatarajiwa kuongeza madarasa matano hadi nane kwa kila shule kutokana na uhitaji wake.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo