Madiwani wamgomea mkuu wa wilaya ya Babati

Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Babati mkoani Manyara, wamemgomea Mkuu wa Wilaya hiyo, Crispin Meela kulihutubia baraza hilo wakidai amekuwa na tabia ya kumnyima ushirikiano Mbunge wa jimbo hilo, Pauline Gekul. 

Hali hiyo ilijitokeza juzi mjini hapa wakati Mkurugenzi wa mji huo, Omari Mkombole alipolieleza baraza hilo kuwa baada ya kufanya uchaguzi wa kuteua kamati, Meela atawahutubia na kutoa maagizo ya Serikali. 

Mbunge wa jimbo hilo, Pauline Gekul alisema hakuna mwongozo wala kanuni ya baraza hilo inayomlazimisha mkuu wa wilaya awahutubie na kumtaka Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Mohamed Kibiki kufunga mkutano bila Meela kuwahutubia. 

Juhudi za Mkombole kuwaomba madiwani hao kukubali mkuu huyo wa wilaya alihutubie baraza hilo hazikuzaa matunda, kwani waligoma na hata walipokaa kama kamati walikataa. 

Akifunga baraza hilo, Kibiki alisema wakati wa uchaguzi Meela alikuwa anaisaidia CCM ishinde na hivi karibuni alifanya kikao na wafanyabiashara wa usafirishaji bila kumshirikisha Gekul. 

Hata hivyo, akizungumzia kuhusu hali hiyo, Meela alisema madiwani hao ambao wengi ni wa Chadema wanafanya vitendo ambayo siyo sahihi kama walivyofanya wabunge wa Ukawa waliotoka nje wakati Rais John Magufuli alipohutubia Bunge. 

Alisema madiwani hao wanatakiwa kutambua kuwa wenyewe wapo chini ya Serikali, hivyo kitendo cha kugoma siyo cha busara kwa kuwa uchaguzi umepita na kwamba, wanachotakiwa ni kuwatumikia wananchi. 

“Kuhusu Gekul kuja ofisini kwangu na kuishia kwa katibu muhtasi, huo ni utaratibu wa ofisi za Serikali kuwa unaeleza shida yako kabla ya kumuona DC na hilo la wafanyabiashara sipaswi kumshirikisha mbunge,” alisema Meela.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo